Utenzi wa Mwana Kupona

Tarehe: Machi 18, 2025 - Kimani wa Mbogo

Huu ni Utenzi wote wa Mwana Kupona (jumla beti 102) kama ulivyorekodiwa katika maandiko ya fasihi ya Kiswahili. Mashairi yamenukuliwa katika lugha ya Kiswahili asili (lafudhi ya Kipate/Kiamu, mwandiko wa kiutendi) bila tafsiri, ili kumwezesha

Utenzi wa Mwana Kupona

  1. Negema wangu binti,
    mchachefu wa sanati
    upulike wasiati
    asa ukanzingatia.
  2. Maradhi yamenshika
    hatta yametimu mwaka
    sikupata kutamka
    neno lema kukwambia.
  3. Ndoo mbee ujilisi
    na wino na qaratasi
    moyoni nina hadithi
    nimependa kukwambia.
  4. Ukisa kutaqarabu
    Bismillahi kutubu
    umsalie Habibu
    na sahabaze pamoya.
  5. Ukisa kulitangaza
    ina la Mola Muweza
    basi tuombe majaza
    Mola tatuwafiqia.
  6. Mwanaadamu si kitu
    na ulimwengu si wetu
    walau hakuna mtu
    ambao atasalia.
  7. Mwanangu twaa waadhi
    pamoya na yangu radhi
    Mngu atakuhifadhi
    akuepue na baa.
  8. Twaa nikupe hirizi
    uifungeto kwa uzi
    uipe na taazizi
    upate kuyangalia.
  9. Nikutungie kindani
    cha lulu na marijani
    nikuvike mke shani
    shingoni kikizagaa.
  10. Penda nikupe kifungo
    kizuri kisicho ongo
    uvae katika shingo
    utaona manufaa.
  11. Yangu utakaposhika
    mwanangu hutosumbuka
    duniani utavuka
    na akhira utakia.
  12. La kwanda kamata dini
    faradhi usiikhini
    na sunna ikimkini
    ni wajibu kuitia.
  13. Pili uwe na adabu
    na ulimi wa thawabu
    uwe mtu mahabubu
    kula utakapongia.
  14. La tatu uwe sadiqi
    wambiwao ulithiqi
    mtu asoshika haqi
    sandamane naye ndia.
  15. Tena mwanangu idhili
    mbee za maqabaili
    uwaonapo mahali
    angusa kuwenukia.
  16. Wangiapo wenukie
    na moyo ufurahie
    kisa uwapeke mbee
    watakapokwenda ndia.
  17. Ifanye mteshiteshi
    kwa maneno yaso ghashi
    wala sifanye ubishi
    watu wakakutukia.
  18. Nena nao kwa mzaha
    yaweteao furaha
    iwapo ya ikraha
    kheri kuinyamalia.
  19. Wala situkue dhana
    kwa mambo usoyaona
    na kwamba na kunong’ona
    tahadhari nakwambia.
  20. Sitangane na watumwa
    illa mwida wa khuduma
    watakuvutia tama
    la buda nimekwambia.
  21. Sandamane na wainga
    wasoyua kuitunga
    ziumbe wasio tanga
    wata kuwaqurubia.
  22. Mama pulika maneno
    kiumbe ni radhi tano
    ndipo apate usono
    wa akhera na dunia.
  23. Nda Mngu na Mtumewe
    baba na mama wayuwe
    na ya tano nda mumewe
    mno imekaririwa.
  24. Naawe radhi mumeo
    siku zote mkaao
    siku mukhitariwao
    awe radhi mekuwea.
  25. Na ufapo wewe mbee
    radhi yake izengee
    wende uitukuzie
    ndipo upatapondia.
  26. Siku ufufuliwao
    nadhari ni ya mumeo
    taulizwa atakao
    ndilo takalotendewa.
  27. Kipenda wende peponi
    utakwenda dalhini
    kinena wende motoni
    huna budi utatiwa.
  28. Keti naye kwa adabu
    usimtie ghadhabu
    akinena simjibu
    itahidi kunyamaa.
  29. Enda naye kwa imani
    atakalo simkhini
    we naye sikindaneni
    ukindani huumia.
  30. Kitoka agana naye
    kingia mkongowee
    kisa umtengezee
    mahala pa kupumua.
  31. Kilala siikukuse
    mwegeme umpapase
    na upepo asikose
    mtu wa kumpepea.
  32. Kivikia simwondoe
    wala sinene kwa yowe
    keti pao siinue
    chamka kakuzengea.
  33. Chamka siimuhuli
    mwandikie maakuli
    na kumtunda mwili
    kumsinga na kumwoa.
  34. Mnyoe mpalilize
    sharafa umtengeze
    na udi umfukize
    bukurata wa ashia.
  35. Mtunde kama kijana
    asiyoyua kunena
    kitu changalie sana
    kitokacho na kungia.
  36. Mpumbaze apumbae
    amriye sikatae
    maovu kieta yeye
    Mngu atakulipia.
  37. Mwanangu siwe mkoo
    tenda kama uonao
    kupea na kosha choo
    sidharau mara moya.
  38. Na kowa na kuisinga
    na nyee zako kufunga
    na asmini kutunga
    na firashani kutia.
  39. Nawe ipambe libasi
    ukae kama arusi
    maguu tia kugesi
    na mikononi makoa.
  40. Na kidani na kifungo
    sitoe katika shingo
    mwili siwate mwingo
    kwa marashi na dalia.
  41. Pete sikose zandani
    hina sikome nyaani
    wanda sitoe matoni
    na nshini kuitia.
  42. Nyumba yako i nadhifu
    mumeo umsharifu
    wakutanapo sufufu
    msifu na kumtaya.
  43. Muyuwe alipendalo
    nawe ufuate lilo
    jambo limtukialo
    siwe mwenye kumwedea.
  44. Na ukitaka kutoka
    sharuti rukhusa taka
    uonapo meudhika
    rudi na kuikalia.
  45. Fuata yake idhini
    awe radhi kwa yaqini
    wala sikae ndiani
    saa yake ikasia.
  46. Wala sinene ndiani
    sifunue shiraani
    mato angalia tini
    na uso untie haya.
  47. Rejea upesi kwako
    ukae na mume wako
    utengeze matandiko
    mupate kuilalia.
  48. Mume wako mtukuze
    sifa zake zieneze
    wala simsharutize
    asichoweza kutoa.
  49. Akupacho mpokee
    na moyo ufurahie
    asolitenda kwa yeye
    huna haja kumwambia.
  50. Uonapo uso wake
    funua meno uteke
    akwambialo lishike
    illa kuasi Jalia.
  51. Mama sinue ulimi
    nioleza wako umi
    nalioa nyaka kumi
    tusitete siku moya.
  52. Alinioa babako
    kwa furaha na ziteko
    tusondoleane mbeko
    siku zote twalokaa.
  53. Siku moya tusitete
    ovu langu asipate
    na lake nisilikute
    hatta akakhitariwa.
  54. Yalipokuya faradhi
    kanikariria radhi
    nkashukuru nkafawidhi
    moyo wangu nkatoshea.
  55. Tangu hapo hatta yeo
    siyanyamaa kilio
    nikumbukapo pumbao
    na wingi wa mazoea.
  56. Watu wakipulikana
    milele hukumbukana
    illa wenye kushindana
    daima huiyutia.
  57. Mausio ya mvuli
    Allah Allah yaamili
    na nduguzo na ahali
    wapende nakuusia.
  58. Uwaonapo swahibu
    ambao wakunaswibu
    wakwambiapo qaribu
    angusa kuqurubia.
  59. Na wachandika chakula
    uchambiwa nawe nla
    wala siweke muhula
    nyumanyuma kurejea.
  60. Wala sifanye kiburi
    mla hata ushakiri
    usiyakuta siqiri
    ukamba ni kondolewa.
  61. Watu wote waumini
    kwako na wawe wendani
    sipende masalatini
    washinde ukiwepua.
  62. Sipende wenye jamali
    na utukufu wa mali
    fuqara ukamdhili
    cheo ukamvundia.
  63. Akupendao mpende
    akuchezo (akuchukizao) mwenende
    kwa zema mvundevunde
    laala akiridhia.
  64. Na ayapo muhitaji
    mama kwako simuhuji
    kwa uwezalo mbuji
    angusa kumtendea.
  65. Mama haya yasikize
    tafadhali sinipuze
    utaona nafuuze
    za akhera na dunia.
  66. Tamati maneno yangu
    kukuusia mwanangu
    sasa ntamuomba Mngu
    anipokelee dua.
  67. Kwani yote ninenao
    mwanaadamu ni pou
    Mola ndiye awezao
    kupoteza na kongoa.
  68. Nakuombawe Manani
    unitilie auni
    ninenayo ulimini
    na yote nisoyatoa.
  69. Yote nimezoyanena
    Rabbi taqabali minna
    na yasalieo tena
    Rabbi Mola nitendea.
  70. Niwekea wangu wana
    na umbu langu mnuna
    yakue yao maina
    yenee majimbo pia.
  71. Rabbi waweke nduzangu
    na wana wa ndugu zangu
    wenee na ulimwengu
    kwa jamala na sitawa.
  72. Na jamii islamu
    Mola wangu warehemu
    matakwa yao yatimu
    na nyoyo kufurahia.
  73. Ya Allahu wangu wana
    nimekupa ni amana
    watunde Mola Rabbana
    siwate kuwangalia.
  74. Nimekupa duniani
    watunde uwakhizini
    unipe kesho peponi
    mbee za Tumwa Nabia.
  75. Wangalie kwa huruma
    waongoze ndia njema
    uwepulie na tama
    za akhira na dunia.
  76. Kukuombawe sikomi
    wala sifumbi ulimi
    ya Mufarrija ’lHammi
    nikomeshee udhia.
  77. Nisimeme muhitaji
    mjao nakutaraji
    alili bi ’l-faraji
    ya afua na afia.
  78. Nondolea ndwe mbovu
    yaloningia kwa nguvu
    dhambi zangu na maovu
    ya Rabbi nighufiria.
  79. Kwetu yangawa mazito
    kwako wewe ni matoto
    nepulia uvukuto
    uepuke mara moya.
  80. Nakuombawe Latifa
    unondolee makhafa
    kwa yaumu ’l-Arafa
    na idi ya udhuhia.
  81. Kwa siku hizi tukufu
    za kuhiji na kutufu
    niafu Rabbi niafu
    unishushize afua.
  82. Ya Allahu ya Allahu
    ya Rabbahu ya Rabbahu
    ya Ghayata Raghbatahu
    nitika hukwamkuwa.
  83. Nakuombawe Rabbana
    bi asmaika ’l-husna
    tisa wa tisiina
    mia kupungua moya.
  84. Nipulishie walimu
    wakinena yafahamu
    dua hini Islamu
    akiomba hujibiwa.
  85. Nami mjao dhaifu
    mwenye nyingi taklifu
    nakuomba takhfifu
    Rabbi nitakhafifia.
  86. Nakuomba taisiri
    mambo nisoyaqadiri
    unegeshe kulla kheri
    shari ukinepulia.
  87. Ya Rabbi nitimiliza
    mambo nisiyoyaweza
    wala moyoni kuwaza
    kwamba yatasikilia.
  88. Rabbi unifurahishe
    mambo mema unegeshe
    maovu uyagurishe
    tusikutane pamoya.
  89. Uniweke duniani
    miongoni ya wahusuni
    nifapo nende peponi
    makao ya hafidhiwa.
  90. Ntungile utungo hunu
    kwa zehemu na zitunu
    kwa qadha yako Dayyanu
    na hukumuzo Jalia.
  91. Ntungile nili saqimu
    moyo usina fahamu
    usomeni Islamu
    mukiogozana ndia.
  92. Na sababu ya kutunga
    si shairi si malenga
    nina kijana muinga
    napenda kumuusia.
  93. Napenda kumnabihi
    laala katanabahi
    kamfuata illahi
    pamwe na wake rijaa.
  94. Somani nyuate huramu
    maana muyafahamu
    musitukue laumu
    mbee za Mola Jalia.
  95. Somani mite ya nganu
    mutii waume wenu
    musipatwe na zitunu
    za akhera na dunia.
  96. Mwenye kutii mvuli
    ndaka jaha na jamali
    kula endapo mahali
    hutangaa yake ndia.
  97. Mwenye kutunga nudhumu
    ni gharibu mwenye hamu
    na ubora wa ithimu
    Rabbi tamghufiria.
  98. Ina lake mufahamu
    ni mtaraji Karimu
    Mwana Kupona Mshamu
    Pate alikozaliwa.
  99. Tarikhiye kwa yaqini
    ni alifu wa miyateni
    khamsa wa sabiini
    hizi zote hijiria.
  100. Na baitize idadi
    ni miati maadudi
    na mbili za mazidadi
    ndizo zimezozidia.
  101. Mola tatusahilia
    kwa baraka za Nabia
    na masahaba pamoya
    dini waliotetea.
  102. Nahimidi nkisalia
    kwa Tume wetu Nabia
    ali zake na dhuria
    itwenee sote pia.

(Asili: Mashairi haya yamenukuliwa kutoka miswada ya asili ya utenzi yaliyochapishwa katika kitabu “Tendi: Traditional Swahili Poems” kilichohaririwa na J. W. T. Allen, 1971.)

193 3

Maoni ya Wasomaji

Bado hakuna maoni yaliyoidhinishwa.

Andika Maoni

Shiriki mawazo yako kwa heshima. Baruapepe yako haitachapishwa wala kuonekana kwa wasomaji.